Mkuu wa Wilaya ya Mufindi, Mhe. Dkt. Linda Salekwa, awahimiza viongozi wa vijiji, viongozi wa dini, viongozi wa Serikali ngazi ya Wilaya pamoja na wananchi kuhamasishana na kujitokeza kwa wingi katika zoezi la usajili na utoaji wa vyeti vya kuzaliwa na vifo.
Wito huo umetolewa Agosti 09, 2026, wakati wa uzinduzi wa kampeni ya usajili na utoaji wa vyeti hivyo uliofanyika katika Ofisi ya Mtendaji wa Kijiji cha Lufana, Wilaya ya Mufindi, mkoani Iringa.
Akizungumza na wananchi katika uzinduzi huo, Dkt. Linda ameeleza kuwa kuwa na cheti cha kuzaliwa au cha kifo kuna umuhimu mkubwa katika nyanja mbalimbali ikiwemo kupata haki za msingi kama vile elimu, Kitambulisho cha Taifa (NIDA), huduma za mikopo ya elimu ya juu, pamoja na masuala ya mirathi.
Katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma hizo kwa urahisi na ukaribu, Wakala wa Usajili, Ufilisi na Udhamini (RITA) umeweka kambi katika Ofisi ya Mtendaji wa Kijiji cha Lufana kwa muda wa siku kumi ukitoa elimu na huduma mbalimbali ikiwemo usajili na upatikanaji wa vyeti vya kuzaliwa na vifo, huduma za ndoa na talaka pamoja na msaada wa kisheria kuhusu kuandika na kuhifadhi Wosia.